MKWASA KULIPWA SAWA NA NOOIJ TSH MIL 25 NA MARUPUPU KIBAO


RAIS wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) Jamal Malinzi amesema kwamba, kocha mpya wa timu ya taifa, Taifa Stars, Charles Boniface Mkwasa atakuwa analipwa sawa na kocha Mholanzi, Mart Nooij aliyeondolewa.
  Nooij aliyekuwa analipwa dola za Kimarekani 12,500 (zaidi ya Sh. Milioni 25) kwa mwezi, alifukuzwa mwishoni mwa wiki baada ya Taifa Stars kufungwa mabao 3-0 na Uganda Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
  Katika Mkutano na Waandishi wa Habari leo, Dar es Salaam, Malinzi amemtangaza rasmi Mkwasa kuwa kocha mpya wa Taifa Stars akisaidiwa na kocha Hemed Morocco.
  Mkwasa ambaye ni Kocha Msaidizi wa Yanga na Morocco kocha wa Mafunzo watafanya kazi kwa kipindi cha miezi mitatu ambayo timu ya taifa itakua na michezo ya kuwania kufuzu kwa CHAN na AFCON.
  Malinzi amesema uteuzi wa makocha hao wazawa umezingatia vigezo vya makocha wa timu ya Taifa kuwa na leseni A ya ukocha kutoka CAF au zinazofanana kutoka mashiriksho mengine duniani wanaozifanyia kazi, jambo ambalo makocha  hao wazawa wamekizi.
  “Kocha Mkwasa atakua akipewa hudumu zote na masilahi  (zikiwemo posho) alizokuwa anapewa kocha aliyeondoka, pia amepewa nafasi ya kuchagua benchi lake la ufundi la kufanya nalo kazi, hivyo nawaomba wadau wa mpira wa miguu na watanzania kwa ujumla tuwape sapoti makocha hao wazawa” aliongeza Malinzi”
  Aidha Kamati ya utendaji ya TFF Iimemteua Alhaj Ahmed Mgoyi kuwa mratibu wa timu ya Taifa, lengo la uteuzi huo wa Mgoyi ni kuwa kiunganishi kati ya kamati ya Utendaji na timu ya Taifa.


EmoticonEmoticon